IWAPO UMEANZISHA THREAD (UZI) JAMIIFORUMS, NA THREAD YAKO IKATIWA KAPUNI NA MODS. JIBU LAKO LIPO KWENYE BLOGU HII. TUPIA UZI HUO ILI TUUWEKE OPENLY TUPIA KWA EMAIL: jamiiforumsblog@gmail.com

Wengine Wanasemaje?

Friday, February 8, 2013

Uchochezi wa Mohamedi Said na dhihaka kwa Wapigania Uhuru wa Tanganyika na Zanzibar

Imeandikwa Na Yericko Nyerere wa JamiiForums.com

Nimesoma maandiko ya ndugu yangu Mohamed Said aliyoyaweka katika kitabu chake akiitacho Historia ya Uhuru upande wa Pili,
Katika maandishi yake ameonyesha wazi kulazimisha dunia iamini kuwa waislamu wamedhulumiwa katika historia ya Uhuru wa nchi hii,
Katika matakwa yake Mohamed Said anataka historia ya Uhuru ingetazama itikadi za kidini kwanza kabla ya kusimamia maudhui halisi ambayo ni Uhuru,

Nikubaliane nae kuwa historia ya nchi yetu inamapungufu na inahitaji masahihisho, lakini kwa hili la Mohamed si masahihisho bali ni upotoshaji mkubwa, Uchochezi na ni Uhaini kwa nchi. Kwa bahati mbaya bwana Mohamed Said histori anayoisimamia ameiakisi kuanzia miaka ya 1950+ tu,

Hajajishughulisha kuutazama utawala wa Kiingereza wala kuutazama upya utawala wa Kijerumani ambao ndio uliosimika misingi ya utawala na mifumo mingi ambayo leo tunaitumia! Mjerumani mfumo wake wa utawala kwa ASILI ni wa kikristu na kwa Tanganyika walisimama hivyo bila kutetereka! (Yaani mfumo kristu 100%)

Akaja Muingereza na yeye mfumo wa utawala wake wa ASILI ni wakikristu!

Imenilazimu kitabu cha bwana Mohamed Said kiitwacho "Maisha na nyakati za Abdulwahid Sykes 1924-1968" (Historia ya uhuru iliyofichwa ya upande pili) kukiita ni NGANO za masika.

Nitaelezea kwa ufupi jinsi kanisa la Tanganyika lilivyoshiriki harakati za ukombozi wa Tanganyika na madhila liliyokumbana nayo.

Ifahamike kuwa vyama vya harakati za ukombozi Tanganyika vilikuwa vingi sana, na vipo vilivyokuwa vikipingana vyenyewe kwa vyenyewe.

Mwaka 1927 – 1929 kanisa Katoliki nchini chini Joseph Gabriel Zelger, lilibainika kuingiza siasa katika utendaji kazi zake, kitendo hiki kiliwakwaza wakuu wa mamlaka ya kikoloni na kupelekea majasusi wakikoloni wapendekeze aachishwe uongozi wa kanisa nchini. Ni kweli tarehe 12 februari 1929 Zelger alistaafu wadhifawake kwa lazima.

Kisa hiki kinasema, Kanisa lilianzisha mafundisho yenye kuchochea fikra za kimaasi, nalilifanikiwa kuandaa wakufunzi maalumu kwenda katika majimbo yote ya kihuduma Tanganyika, hilo lilipelekea kuleta mtafaruku na dola ya mkoloni wa kiingereza ambapo ilimgharimu kiongozi huyu wa kiroho kuachia madaraka yake.

Alipoingia askofu Edger Aristide Maranta mwaka 1930, ikiwa kama vile mwendelezo wa mtangulizi wake, Askofu Maranda alianzisha harakati za kuwashawishi viongozi wengine wa majimbo kuendeleza kutoa mafundisho yenye kumfanya mtanganyika ajitambue na adai uhuru wake,

Mfano: 23 mei 1938 wakati makanisa saba ya Kilutheri yakiwa kwenye hatua za mwanzo za mchakato wa kuungana, Askofu maranda aliomba kuhudhuria kikao cha tarehe 8 mwezi wa sita kilichofanyika Mjini Arusha, Askofu Maranda aliudokeza mpango ule wa siri wa katoliki katika kikao hicho, japokuwa kulikuwa na hofu ya kutoaminiana, lakini uthabiti wa malengo hayo ulijipembua baadae na kuwa wamafaa.

Juhudi za kanisa kupigania ukombozi ziliendelea kushika kasi huku zikiendeshwa kwa siri sana kwamfumo wa neno la kiroho, na ilipofikia miaka ya 1950+ kanisa sasa lilikuwa tayari linanguvu ya ushawishi kufuatia mafanikio ya harakati za kanisa katika nyanja za ukombozi barani afrika.

Mtihani mkubwa kwa kanisa ilikuwa ni namna gani linaweza kuingia rasmi kudai uhuru wa Tanganyika. Katika kipindi hiki tangu harakati za kanisa zianze, Askofu Maranta pamoja na mapadre wa baadhi ya mikoa, walikuwa tayari ameshafanya juhudi kadhaa za kukutana na Mashehe waliokuwa na ushawishi mkubwa, mfano 05/02/1948, Askofu Maranda alikutana Shehe Issa bin Amir kiongozi wa kiroho katika msikiti wa Ilala - mchikichini. Mazungumzo yao yalihusu harakati za ukombozi, Shehe Issa alimshauri Askofu kuwa ikiwa makanisa na misikiti yanapigwa marufuku na mkoloni kujihusisha na siasa za ukombozi basi watafute baadhi ya vyama vya harakati za ukombozi na waviunge mkono, wazo hilo lilimvutia Askofu lakini akajenga hofu kama je ndani ya vyama hivyo watapata vijana wasomi?.

Siku chache baada ya makutano yake na Shehe Issa, Askofu Maranta aliletewa mapendekezo kutoka kwa Attilio Beltramino kassi wa katoliki aliyehudumu kule Iringa, mapendekezo ya kasisi huyu yalikuwa ni, Umishonari makao makuu uruhusu udurufu wa biblia zisomeke kwa makabila ya wahusika wa eneo, ndani ya biblia hizo yaongezwe mafundisho ya haki ya kujitambua na kujitawala wenyewe. Pendekezo hili lilimvutia sana Maranta hivyo akalipa baraka zake, kwa hakika lilifanikiwa na ndio lilizaa hisia kali za mwamko wa kudai uhuru, mfano biblia ya lugha ya kihehe ilikuwa inaeleza wazi athari za kutawaliwa.

Harakati za Ukombozi za Mwalimu Nyerere zililivutia kanisa na likaamua kumuunga mkono, mfano mwaka 1953 wakati TAA kikiwa chama chenye nguvu, Askofu Maranta alimwalika ofisini kwake Mwalimu Nyerere, walizungumza mengi lakini kubwa nikuwa alimsifu kwa juhudi za kujipambanua bila kuwaogopa wakoloni na akamweleza jinsi kanisa linavyounga mkono juhudi za ukombozi wa Tanganyika, kisha akamshauri kuwa ajaribu kuvishawishi baadhi ya vyama vya harakati za ukombozi viungane ili kuvipa nguvu ya kudai uhuru na kanisa litasaidia.

Wazo la Askofu Maranta lilimkaa Mzee Nyerere na mwaka 1954, alianza juhudi za kuwaunganisha vijana wenzake wa kariakoo ambao walikuwa ndani ya TAA na wenye nguvu ya ushawishi lakini wakikabiliwa na matatizo makubwa mawili katika lengo lao.



Elimu,

Woga



Ikumbukwe kuwa mwaka 1953 baada ya harakati za ukombozi kupamba moto na kamata kamata ya wanaukombozi, Askofu Edger Aristide Maranta alihamishiwa Zanzibar na nafasi yake ikachukuliwa na Vicar Apostolic, lakini bado aliendelea kuwa mshauri imara wa Mwalimu Nyerere. Jambo la kushangaza kama si kufurahisha, mwaka huohuo mwezi wa 8, Edger Aristide Maranta alirudishwa tena Dar es Saalam, na sasa mbinyo dhidi ya ukoloni ikahika mkondo wake.

Mnamo tarehe 7/71954, Vijana (wazee wa kariakoo) wakiongozwa na Julius Kambarage Nyerere, walikubaliana wazo la kuhuisha chama kutoka TAA kwenda TANU, chini ya uratibu wa karibu wa kanisa Katoliki (Askofu Maranta) na Waislamu (Shehe Issa bin Amir)


Mpaka hapo ndugu yangu Mohamed Said angalau umepata picha kwa KIFUPI tu ya harakati za uhuru chini ya kanisa.

Nikipata wasaa nitakuletea picha za Mwalimu Nyerere na Edger Aristide Maranta

Kwanini Kasisi huyu wa kikatoliki Edger Aristide Maranta hatajwi popote katika historia ya nchi? Kwanini kanisa katoliki halilalamiki kutokuwepo kwenye kitabu cha kivuko?

Yote hayo nitakushushia taratibu kadiri mnakasha huu unavyoenda.

Sasa nini kilifuata baada ya uhuru?

Nitaeleza kwakifupi tu:

Mwalimu Nyerere baada ya kukabidhiwa mamlaka kamili ya kushika dola na Malkia wa Uingereza alianza mageuzi ya kubadili mfumo huo kristu hasa mwanzoni mwa 1962 na juuhudi zilishika kasi zaidi mwanzoni mwa 1964 baada ya kuunganisha nchi ya Tanganyika na Zanzibar na kuzaliwa kwa Tanzania!

Juhudi hizi zilikwenda taratibu na kwa ufanisi wa hali ya juu kwakupitia hatua kadhaa ambazo ni pamoja na, kutaifisha huduma za kijamii zote zilizokuwa chini ya makanisa, kuanzisha sera ya elimu ya msingi kuwa ni ya LAAZIMA kwa watanzania wote nk, Kumbuka Mjerumani amekaa zaidi ya karne tatu akitumia mfumo kristu kutawala, Muingereza nae akalowea karne kadhaa akitawala kwa mfumo huohuo, Lakini ndani ya miongo miwili tu ya utawala wa Mwalimu Nyerere huku nchi ikitoka kwenye dimbwi la ukoloni aliweza kubadili sura na mfumo huo wa kikoloni na kuwa wawatanzania wote bila kujali dini, kabila rangi au kanda.

Naomba nimfungue macho na akili rasmi Mzee Mohamed Said huyu mpigania Dini kwa mgongo wa Uhuru wa nchi hii.
Nitaeleza kwa kifupi tu yale anayoyalilia Mohamed Said juu ya WAZEE wake.


Ukweli nikuwa kuanzia mwaka 1955 kulianza kuibuka mlengo tofauti kwa baadhi ya washarika wa ukombozi ndani ya TANU,
Hasa hasa mlengo huo ulikuwa ni kuweka itikadi ya DINI mbele, yaani iwe ndio tiketi halisi yakupigania uhuru na sio Utanganyika wao, na baada tu ya kupata uhuru, baadhi ya wazee waliokuwa beba kwa bega na Mwalimu katika harakati za kudai uhuru WALIASI rasmi sera ya Mwalimu nakuanza kuendesha vita ya chini kwa chini yakumpindua Mwalimu chini DINI.

Mwalimu Nyerere kwakutumia falsafa na malengo yake ya tangu akiwa Shule ya Tabora, Chuo kikuu Makerere na pale Scotland akiwa sambamba na wanaukombozi wasomi wenzie waliweza kuanzisha mfumo stahiki wa kufuta UDINI, UKABILA, Rangi, Ukanda na kisha Waliamua kuwafanya Watanganyika kuwa kitu KIMOJA.

Sasa mgogoro ulikuja kwa WAASI, kwakuwa hawakukubaliana na sera za Serikali mpya ya Mwalimu, wakaziidisha vurugu kwakushawishi makundi kadhaa ya kiroho yaenzi uasi huo, hilo lilipelekea serikali kuchukua hatua madhubuti dhidi yao ambapo mwaka 1962 katika kiwango cha juu cha hekima za Mwalimu Julius Kambarage Nyerere na waambata wake, waliamua kuanzisha sheria ya kumuweka mtu kizuizini.

Sheria hii ilikuwa na mafaa kwa waasi kwani ililinda hadhi zao licha yakuwa waasi waliostahili vifungo vya maisha au kunyongwa kama ilivyokuwa destuli ya viongozi wengi wa dunia ya pili.
Mashehe wengi walitiwa kizuizini na wengine kufukuzwa nchini na makasisi wengi kupewa onyo kali.
Ifahamike kuwa hilo halikuwakumba mashehe tu kwani uasi huo ulikuwa hata kwa makasisi waliotaka itikadi zao ipewe kipaumbele zaidi na serikali ya Mwalimu Nyerere.

Kazi aliyofanya mzee Nyerere ni kubwa na alikumbana na vikwazo vingi sana kutoka kwa wakatoliki, rejea kitabu cha Van Bergen kuna barua nzito ya Mwalimu Nyerere kwenye faharasi ya 15 kwenda kwa makasisi wa kikatoliki akiwatolea karipio kuu kwakukwamisha juhudi zake, katika hii hakuchukua karne kadhaa kuumaliza mfumo uliodumu kwa mvua na mvua.

Japokuwa hakumaliza chembe za mfumo huu lakini kwangu naona ni zaidi ya 98% alimaliza, palipobaki ni mimi, wewe na wale ndio wenye dhamana ya kumalizia.

Uthabiti na tunu aliyoifanya Mzee Nyerere inathibitishwa kwa Hotuba yake ya tarehe 5 Novemba, 1985 kabla hajastaafu urais, Mzee Nyerere aliwahutubia wazee wa Dar es Salaam. Hotuba hii ilikuwa thabiti na yenye kuvuta nyoyo za waungwa, Baba wa Taifa Mzee Nyerere akikumbuka jinsi Waislam walivyompokea Dar es Salaam kwa mapenzi makubwa ingawa yeye alikuwa Mkristo. Wazee hawa wakiwemo Bin Amir ambae Mohamed Said anamlilia, wengi wao walikuwa wanachama wa zamani wa TANU waliomuunga mkono Nyerere wakati wa kudai uhuru. Mzee Nyerere aliusifia mchango wa Waislam katika kipindi kile kigumu cha kudai uhuru. Nyerere alisemakuwa "upogo katika elimu uliorithiwa na serikali yake kutoka kwa Waingereza baina ya Waislam na Wakristo yeye ameuondosha katika kipindi cha utawala wake":

Inakera kuona wewe Mohamed unarudisha nyuma juhudi za wanaukombozi wetu na kupandikiza chuki miongoni mwa dini hizi mbili!
Faida unayopata ni ndogo na niyakwako tu kuliko hatari inayolikumba taifa hivi leo!
Sipingi kusahihisha historia ya nchi hasa kama kuna mema yaliyoachwa lakini kupotosha na kuchochea kunatulazimisha tuhoji mamlamla za usalama wa nchi zimelala wapi? Leo mapinduzi matukufu ya Zanzibar, Mohamed Said anataka kutuaminisha kuwa Wanamapinduzi hawa wa Zanzibar waliwadhulumu waislamu wa Zanzibar na kuweka mfumo kristu anaodai upo au mfumo huo upo kwa Tanganyika tu?!


Katika kitabu chake bwana Mohamedi ametoa shutuma nyingi sana kwa Hayati baba wa Taifa Mwalimu Julius Kambarage Nyerere ikiwemo ya eti Mwalimu katika hotuba yake ya kuaga taifa alitamka wazi kuwa hamjui ABDUL SYKES, Inashangaza sana kwani Mohamed Said anajua wazi ameudanganya umma na kudhihaki wanaukombozi wetu.

Ilikujiridhisha ndugu zangu wadau pitieni sehemu ya Hotuba ya Mwalimu Nyerere ya kuaga taifa tarehe 5 Novemba, 1985 kabla hajastaafu urais aliyoitoa mbele ya wazee wa Dar es Salaam,




‘"Mimi nimeanza siasa na wazee wa Dar es Salaam; na wazee wa Tanzania. Nimeanza nao mapema sana; mapema kweli. Nilirudi kutoka masomoni, Uingereza Oktoba 1952 – miaka 33 nyuma. Wakati huo nikiwa kijana mdogo wa miaka thelathini na kidogo hivi.

Niliporudi nikakubaliana na wamisionari hapo Pugu (sekondari), nifundishe shuleni kwao. Lakini nikiwa shuleni – Chuo Kikuu – nilijua. Niliishaamua kwamba maisha yangu yatakuwa ya siasa. Niliamua hivyo: Nitafundisha kwa muda wa miaka mitatu, nione hali inavyokwenda na kuzoeana na wenzangu kabla ya kuanza maisha ya siasa.

Niliporejea nchini hapo Oktoba, nikaenda Butiama. Januari nikarudi Dar es Salaam. Nikaanza kazi. Nikataka kujua habari za African Association. Mzee Mwangosi anakumbuka. Yeye ndiye aliniambia habari za African Association. Aliisha niambia habari hizo tangu nikiwa Makerere – Chuo Kikuu – nikiwa mwanafunzi.

Pale, mimi na wanafunzi wenzangu tulikuwa tumeanzisha chama kinachoitwa Tanganyika African Welfare Association (TAWA) cha wanafunzi wa Tanganyika; mimi nikiwa katibu wao. Hapa tukaona mambo yanakwenda vizuri kidogo.

Tukaona kwanini TAWA iwe ya wanafunzi peke yao na siyo Tanganyika nzima. Kwa hiyo nikawaandikia baadhi ya watu Tanganyika. Nikasema, jamani ee, tumeanzisha chama, kwanini msianzishe huko matawi ya chama hicho?

Ndugu Mwangosi akapata barua hiyo. Alikuwa miongoni mwa waliopata barua hiyo. Akaniandikia – nikiwa Makerere – akasema: wewe kwanini unataka kuanzisha chama kipya? Kipo chama. Kipo chama cha TAA (Tanganyika African Association).

Kwa hiyo la maana siyo kuanzisha matawi, maana chama kipo na matawi yameenea; la maana ni kwamba hicho chama chenu mfute, na muanzishe tawi la Tanganyika African Association.

KUVUNJWA KWA TAWA

Hivyo ndivyo tulivyofanya. Kwa hiyo mimi nikawa katibu wa katawi ka TAA hapo Makerere. Niliporudi Tabora na kuanza kufundisha pale St. Marys (sasa inaitwa Sekondari ya Milambo), nikachaguliwa katibu wa TAA wa jimbo ambalo makao yake makuu yalikuwa Tabora. Ulipofanyika mkutano wa TAA mjini Dar es Salaam, nilihudhuria nikiwa mjumbe kutoka Tabora.

Kwa hiyo nilikuwa naijua Tanganyika African Association. Nilipokuwa ninaondoka kwenda Ulaya kusoma, nilikuwa nimeishaonja shughuli za TAA. Sasa niliporudi, baada ya kukaa Pugu siku chache, nikaja mjini Dar es Salaam. Nikauliza nani wanaongoza TAA?
Nikaambiwa kuna jamaa mmoja anaitwa Abdul Sykes. Sasa ni marehemu. Abdul ndiye alikuwa katibu wakati huo.

Nilipelekwa na Kasela Bantu - ambaye naye aliteleza-teleza na hatunaye hapa (kwenye mkutano). Kasela Bantu alikuwa mwalimu mwenzangu. Tulifundisha pamoja Milambo. Nilipokuja Dar es Salaam, nikakuta anafanya kazi Redio (Tanganyika Broadcasting Corporation). Ni Kasela Bantu aliyenipeleka kwa Sykes.

Wakati huo mambo yalikuwa yanasinzia kidogo. Kwa muda mfupi mwaka ule, tukafufua-fufua, hasa kutoka Januari. Kufika Aprili, TAA ikafufuka. Tukafanya mkutano hapo Anautouglou. Kwenye mkutano huu wakanichagua kuwa Rais wao – wa TAA.

Ninasema yote haya kwa shukrani kwa wazee. Jamaa hawa walikuwa watu wazima wa Dar es Salaam, na mimi kijana mdogo Mzanaki, na Kiswahili changu si kizuri sana – cha matatizo.

Nimekuja, natoka Ulaya, tena masomoni. Muda mfupi tu jamaa hawa wakaniamini haraka sana – katika muda wa miezi mitatu. Wakanichagua Rais wa TAA. Hapo ndipo nilianza shughuli mpya ya kuandika katiba ya TAA na kuipa madhumuni hasa ya shabaha ya kuleta uhuru.

Baada ya miezi 13, hapo 1954, tukaanzisha TANU. Jina hili lilipendekezwa na akina Abdul Sykes. Walikuwa wamelifikiria tangu zamani, walipokuwa askari vitani huko Burma (Vita vya Pili).

WAZEE NA MSIMAMO

Miezi minne baada ya kuanza kazi Pugu nikawa ninakuja Dar es Salaam, kwa mguu; kila Jumamosi. Baadaye wazee wakanipa baiskeli nikawa ninakuja mjini kukutana na wenzangu; kufanya mikutano.

Hivyo ndivyo tulivyofanya. Wazee wakaniamini upesi sana. Tukawa na uhusiano mkubwa sana. Wadogo wenzangu wengine walikuwa Abdul Sykes, Abass Sykes (mdogo wake), Dosa Aziz – waliokuwa wengi ni wazee.

Katika kuhutubia mikutano yangu, nilikuwa nikisema: Wazee na Ndugu zangu! Wazee hasa ndio walikuwa na mikutano ya awali ya TAA na TANU. Walikuwa na msimamo wa hali ya juu kabisa! Hawakuyumba hata kidogo! Vijana walikuwa na mashaka. Wengine walikuwa na vikazi vyao, waliogopa kuvipoteza.

Nalo jambo lenyewe ni la hatari – la kuzungumzia uhuru! Unaweza ukakosa kazi; na wapo waliopoteza kazi; wengine wakaacha kazi. Akina Rashid (Kawawa) waliona watoke kwenye shughuli hizo tuje tuungane katika chama.

Wazee wa Dar es Salaam, na baadaye wa nchi nzima, wakatuunga mkono, na kila nilipokwenda, watu wa kwanza walionielewa, walikuwa wazee.

Nilikwenda Songea mwaka 1955 mara baada ya kujiuzulu. Huko wazee walinipokea na kunielewa. Nilianza safari za kuitembelea Tanganyika nzima. Nilikwenda Mbeya. Mkutano wangu niliufanya na wazee; kikundi kidogo cha wazee, ndani ya nyumba ya mtu.

Kwa mkutano huu wa Mbeya, wazee wakauliza: Unatafuta nini? Nikawaambia natafuta uhuru. Wale wazee, kwa sababu ya vita vya Maji Maji, na wanakumbuka, kabisa, wakaona mimi ninatafuta jambo la hatari. Tulifanya mkutano wa makini kweli. Wakauliza: Wewe unawezaje kuleta uhuru? Wewe una njia gani kudai uhuru na usitiwe kitanzi na Waingereza?

WAINGEREZA WAONGO

Tulielezana. Nikawaambia ninyi wazee, Waingereza wanawadanganya, Waingereza wametumwa na ule Umoja wa Mataifa uliokufa (League of Nations), waje kuishika Tanganyika kwa muda tu; watusaidie, na wakati tutakapokuwa tayari, watuachie tukajitawale.

Waingereza wanafanya ujanja; hawasemi. Vita vimekwisha (vya Pili) na Umoja wa Mataifa mwingine – mpya (United Nations Organisation – UNO) umewakabidhi Tanganyika kwa shabaha ileile. Sisi siyo koloni lao. Wamepewa dhamana tu.


Kwa hiyo nikawaambia wazee, hakuna haja ya kumwaga damu. Tuwaseme tu! Tuwashitaki kwa waliowaleta hapa kwamba hawafanyi kazi yao; wamesahau kabisa!

Wazee wakauliza: Eh, inawezekana? Nikasema inawezekana. Kazi yetu ya kwanza ilikuwa kuwaambia watu kwamba uwezekano wa kujitawala upo. Hilo lilikuwa la kwanza. Wazee walijua maana ya kujitawala. Walitamani kujitawala, lakini hawakujua waanzie wapi.

Vijana hawakuwa na habari kwamba kujitawala kunawezekana. Kwa hiyo kwa wazee sikuwa na matatizo. Wao hawakuwa na kazi; hawakumwogopa Mwingereza. Hawakuogopa kufukuzwa kazi. Baadhi walikuwa wafanyabiashara.

Mzee John Rupia (marehemu) alikwua mfanyabiashara na kaidi kidogo. Aliwahi kutishwa na kunyang’anywa leseni yake ya biashara. Akaambiwa akiendelea kushirikiana na kijana mwenda wazimu (Julius Nyerere), atanyang’anywa leseni moja kwa moja. Rupia aliwajibu: Potelea mbali!

Nasema yote haya ikiwa njia ya kutoa shukrani kwa wazee na imani yao kwa vijana wakati huo.

Imani hujenga imani. Na mambo haya makubwa ya nchi, kama hayana baraka za wazee hayaendi. Magumu sana. Wanasema ngoma ya watoto haikeshi! Mimi nilipata baraka za wazee tangu zamani. Tangu awali kabisa.

TWAININGI AMEKWISHA

Siku moja, Dosa akanifuata Magomeni (Dar es Salaam). Akasema: Leo wazee wanakutaka. Wapi? Kwa Mzee Jumbe Tambaza. Wanakutaka usiku. Nikasema haya, nitakuja. Nikaenda. Nikakuta wazee wameshakaa; wameniita kijana wao kuniombea dua. Mimi Mkristo, wao Waislamu watupu. Wakaniombea dua za ubani. Tukamaliza.

Tulipomaliza wakasema kuna dua pia za wazee wao. Basi wakanitoa nje. Tukatoka. Zilipomalizika zilikuwa za Korani; sasa zikaja dua za wazee – za jadi.

Walikuwa na beberu la mbuzi. Wamechimba shimo. Wakaniambia simama. Nikasimama. Beberu akachinjwa, huku anaambiwa, “Twining (Twainingi) umekwisha!” (Edward Twining alikuwa Gavana wakati huo). Ndipo nikaambiwa: Tambuka! Nikavuka lile shimo. Hapo nikaambiwa na wazee: Basi nenda zako; tangu leo Twainingi amekwisha!

Sasa mimi Mkristo; hao Waislamu. Na mimi mkorofi-korofi katika mambo haya (ya kutambika). Lakini tulikuwa tunaelewana na wazee wangu hao. Kwa hiyo nilitambuka pale na kuambiwa: Nenda nyumbani salama. Twaining hawezi tena!

Wazee wangu wengine wanakumbuka tulikuwa tunakwenda Bagamoyo. Kwenye makaburi kule! Tunapiga dua huko kwenye makaburi na wazee wangu.

Baadhi yetu mtakumbuka safari moja jamaa wa Kenya, hawa akina Tom Mboya (marehemu) walishitakiwa. Tukasema tuwasaidie. Tuwasaidie vipi? Tukasema tufunge. Tukaomba nchi nzima kufunga siku hiyo. Tufunge! Tukafunga. Hakuna kula. Na siku ya kufunga tulikuwa na mkutano Bagamoyo. Tukaenda huko. Tukafanya mkutano hadi saa 12 jioni.

Baada ya mkutano tukaenda nyumbani kwa Mzee Mohamed Ramia (marehemu). Hapa ndipo tulikuwa tumefikia. Mimi nikamuuliza mzee: Sheikh, una Aspro? Akajibu: Kwa nini unataka Aspro? Nikajibu kuwa kichwa kinaniuma kwelikweli. Akasema subiri.

Tulisubiri hadi saa ya kufuturu. Tukafuturu vizuri. Mzee Ramia akaniuliza: bado unataka Aspro? Nikajibu kichwa sasa hakiumi. Kumbe ilikuwa njaa.

Nawaelezeni haya kwa sababu huko tulikotoka, tulishikamana sana. Tulishirikiana sana na wazee."’



Mohamed Said kuwa mkweli, waambie ukweli watanzania (waislamu) kuwa umetumia mgongo wa Uislamu na Hayati Abdul Sykes, kwakumkashifu na kumdhihaki Hayati Mwalimu Julius Nyerere na kuwasafisha wazee wako walioasi serikali mpya ya Mwalimu ambapo ndipo madhila hayo wakayapata.

Juzi nimemuuliza maswali katika mjadala flani hapa, lakini majibu yake yamenifanya nijiridhishe kuwa Mohamed Said ni muhaini na mchochezi mkubwa wa nchi hii, Ameudhihaki Uislamu nchini na duniani kote,

Nilimuuliza hivi:


Naomba unijibu maswali haya kwaufasaha mwanazuoni Mohamed Said:

1) Uliathirika vipi kwa baadhi ya wazee waliopigania uhuru wa nchi hii kutokuwemo kwao katika histori ya nchi hii kama unavyodai?

2) Taifa na waislamu waliathirika vipi kwa baadhi ya wazee unaodai wewe walipigania uhuru wa nchi hii na hawamo katika historia?

3) Ulijuaje kuwa wazee hao walipigania uhuru ilihali hawapo katika historia stahiki ya nchi hii?

4) Unaposema historia ya uhuru wa nchi hii haiwakumbuki ama haiwatambui, ulitaka wakumbukwe katika maandishi ya vitabu au katika nyaraka za serikali za historia ya uhuru wetu?

5) Unatambua kuwa historia ya nchi yoyote ile duniani huwa wapi?

6) Upeo wako umegota kwenye historia ya waislamu wa Tanganyika na Nyerere tu, au historia ya waslamu duniani kote? Kama ndivyo, je matatizo ya waislamu wa Nigeria, Somalia, Sudani, nk Nyerere ndiye kayapeleka?

7) Je ulichokiandika ni historia ya Uhuru wa Tanganyika au ni historia ya baadhi ya Waislamu wa Tanganyika na mapito yao kisiasa?

8) Kwanini unaulazimisha umma kwa maandishi yako uamini kuwa ulichoandika ndio historia sahihi ya Uhuru wa Tanganyika?

9) Je ni kweli Mohamed Said huwajui na huwatambui wale wazee 17 waliosimama kidete kudai uhuru wa nchi yetu? Je wote walikuwa wakrstu?

Naomba majibu ili tujenge hoja mpya yamjadala huu kwa mafaa ya taifa letu!




Quote By Mohamed Said View Post
Yericko Nyerere,


1) Nimeathirika kwa kuona wazee wangu hawamo katika historia kwa hiyo hawatakuwamo katika kumbukumbu kama mashujaa wazalendo waliopigana kuung'oa ukoloni Tanganyika.

2) (Hilo la taifa sina haki ya kulijibu watajibu wenyewe wenye mamlaka mimi nitawajibia Waislam). Kizazi kijacho hakitajua ushujaa wa Waislam katika kupinga dhulma kama moja ya mafunzo ya Allah. Pili hawatajua nguvu iliyokuwapo katika Uislam Tanganyika katika karne ya 20 nguvu iliyopelekea kupigana na Wajerumani katika vita vya Maji Maji 1905.

3) Babu yangu Salum Abdallah alikuwa katika African Association na TANU na aliongoza mgomo (general strike) ya 1947 Tabora na 1953 yeye na wenzake walifanya mkutano wa mwisho na wa siri wa TAA kutayarisha mjumbe Germano Pacha kuhudhuria kuasisiwa kwa TANU Dar es Salaam 7 Julai 1954. Juu ya haya alikuwa mmoja wa wafadhili wa chama. 1955 aliasisi Tanganyika Railway African Union (TRAU) akiwa mwenyekiti wa kwanza. 1960 aliongoza mgomo wa Railway uliodumu siku 82. Huu hadi leo umebaki mgomo wa kihistoria hawajaweza wafanyakazi kugoma kwa miezi 3.

4) Nilitegemea Nyerere angeliwaadhimisha katika uhai wake angalau kwa kuwataja au kuwapa heshima zao stahiki lakini akawa anakebehi juhudi za TAA na kufikia kusema kuwa hakumbuki Abdulwahid Sykes alikuwa na nafasi gani katika chama yeye alipoingia TAA Dar es Salaam mwaka 1953. (Nikawa na taarifa nyingine kuwa hakuwa anapenda Waislam wahisishwe na juhudi za kuikomba Tangnayika au yeye binafsi kuhusishwa na Abdu Sykes, Kiyate Mshumi, Sheikh Hassan bin Amir, Sheikh Suleiman Takadir na wengine wengi.) Kabla ya kustaafu alitoa medali 3, 979 kuwaadhimisha Watanzania walioifanyia makubwa nchi yetu. Hata mmoja katika wale waliopigania uhuru wa Tanganyika alikuwa katika ile orodha.

5) (Sijalielewa swali labda unifafanulie).

6) Najua mengi kiasi changu katika historia ya Uislam duniani lakini kitabu changu ni kuhusu Waislam wa Tanganyika.

7) Nilichoandika ni historia ya uhuru wa Tanganyika na mchango wa Waislam katika vita ile. Jina la kitabu linajieleza.

8) Huwezi kulazimisha watu sina uwezo huo nilichoandika ni historia ya wazee wangu wakati wa kupigania uhuru. Halikadhalika sina uwezo wa kulazimisha vyuo vinialike. Naalikwa kwa kuwa wameona watanufaika na elimu yangu katika somo hilo.

9) Nawatambua wote 17 na najua hadi historia zao. Kuna wengine walistahili wawepo katika ile orodha ya waasisi wa TANU lakini hakuwapo kwa kuwa mkutano usingeweza kuhudhuriwa na kila mtu. Mfano Sheikh Hassan bin Amir, Dk. Michael Lugazia, Ali Migeyo, Hamza Mwapachu na wengine wengi.

Lakini maswali mengine yamsingi yaliulizwa na wadau wengi kama Nguruvi3, Mwanakijiji na moja ya maswali yaliyonivutia ni hapa hapa chini:


By adolay:


Ninakuuliza somalia na nyerere kwasababu waislam wa somalia wanamatatizo makubwa ya kijamii, kisiasa, kieliemu, afya nk

Nani mchawi maana hapa kwetu kwa mujibu wa hadithi zako ni Nyerere. (Tunaongelea matatizo ya waislamu na wanaowahujumu)

Watanzania (Waislam, wakristu pia wa imani zingine na wasio amini) wanamatatizo aghalabu si makubwa kama ya wasomali.

1. Kwanini useme waislam wa Tanzania ni hujuma za nyerere na kwanini wasiwe waislam wa somalia? kunatofauti ya uislam wa somalia na ule wa tanzania?

2. Je katika historia yako ufahamu wako umegota Tanzania kwa hayati JK Nyerere peke yake? kama ndivyo nini ubora na ufahamu wako kujisifu mwanahistoria makini kama sio mbabaishaji?

Tafadhali rejea maswali kutushawishi kwamba wewe ni mkweli na kashifa zako dhidi ya Nyerere ni uwongo na majungu.

Tuanze na Somalia, nataka usome swali uelewe ujibu kama nilivyouliza sio kuniwekea hadithi za maandishi zisizoakisi maudhui ya swali.

1. Nani amewahujumu/aliwahujumu wasomali na uislamu wa somalia mpaka wamefikia hapa walipo je? ni nyerere

2. Ni mfumogani unatumika katika kuitawala somalia kiasi kwamba wamefika hapo walipo ilituutupie lawama

a) Mfumo kristo ndiyo maana wamefika hapo walipo

b) Mfumo islam, mahakama ya kadhi nk

c) hufahamu nakama hufahamu nini mtazamo wako.

Ninakuuliza maswali haya lengo nikutaka kuujuwa ukweli wa pengine Nyerere huyu pia yupo somalia, afghanistan, pakistani, lebanon, syria, libya nk nakwamba machafuko yote yanayoendelea huko ni hujuma za Nyerere na mfumo kristo kama unavyowapotosha watanzania na kuwachochea!

Naomba majibu ya maswali yangu hapo juu kuthibitisha kwamba wewe sio mchochezi na mchonganishi wa waislamu na wakristo kwa kubuni vitu visivokuwepo.

Mohamed Said, baada ya utangulizi huo narejerea maswali yangu ya jana kwa ufafanuzi. Angalizo jibu maswali kama yalivyoulizwa na sio siasa au funika kombe mwanaharamu apite kwa nukuu za maandishi zisizobeba maana wala majibu ya hayo maswali




MAJIBU YA MOHAMED SAID:

By Mohamed Said
Umeingiza mambo mengi sana.
Kuna Zanzibar, elimu ya Waislam, matokeo mabaya ya shule za Kiislam, kuchinja.

Itakuwa tabu kufanya mjadala uliokuwa hauna mwelekeo ulionyooka.

Lakini kwa mukhtasari ukitaka historia ya Zanzibar na maendeleo yake itabidi tuanza kwa kuvamiwa
kwa Zanzibar na jeshi mamluki la Wamakonde kutoka Kipumbwi wakifadhiliwa na utawala wa Nyerere.

Kuanzia hapa tutaingia katika tatizo la Muungano na kwa nini leo Wazanzibari wanadai nchi yao.

Kuhusu elimu ya Waislam itatubidi tuje katika njama za Nyerere kuhujumu chuo kikuu cha Kiislam
kilichokuwa kijengwe Dar es Salaam mwaka 1968 na jinsi alivyotumia uongo na ghilba kuvunja EAMWS
na kuunda taasisi kibaraka BAKWATA.

Vipi shule za Waislam hazifanyi vyema inabidi tuje katika hujma ya NECTA kwa wanafunzi wa Kiislam na
tuupitie waraka wa marehemu Prof. Malima kuhusu yale aliyoyakuta Wizara ya Elimu mwaka 1987.

Wizara ya Elimu na NECTA vimegeuzwa vigango vya kanisa.

Kubwa zaidi ni kuwa Waislam kwa muda mrefu hatukuruhusiwa kujioganaizi nje ya BAKWATA kibaraka
wa serikali.

Makanisa mnaendelea kwa kupendelewa na serikali iliyojaza watendaji Wakristo sisi tungepewa hayo
mabilioni ya MoU kati ya Makanisa na Serikali tusingekuwa kama hivi.

Yapo mengi sasa chagua tuanze na lipi katika hayo hapu juu niliyokugusia.

Wajerumani waliwaweka Wayahudi katika ghetto kisha wakawa wanawalaumu kwa uchafu.
Kwenye ghetto hakuna maji wala misala sasa watu wafanyeje?

Mnatusimanga kwa hospitali mnazoendesha kwa hela ya kodi ya serikali kodi inayolipwa na raia
wote.

Tunabanwa na mfumokristo kisha mnatulaumu hatuna maendeleo







Mohamed said

katika pita pita zangu nimekutana na post yako hii ya tare 4 January 2013 #914

Umeongelea kunyanyaswa kwa waislamu katika elimu ni njama ya JK Nyerere - Elimu ya somalia ipo taabani sana na Nyerere hayupo huko

Nakwamba Nyerere alitumia uongo na ghilba kuvunja EAMWS - lakini ghilba wala uongo wa nyerere haupo Somali na inateketea vibaya

Necta imegeuka vigango vya kanisa - Somalia haina vigango vya makanisa katika taasisi zake hususani elimu lakini ipo taabani

Serikali imejaza wakristo kwa upendeleo na kuwaacha waislam - Somalia serikali takribani yote ni waislam hakuna maendeleo

Wakristo
wanawasimanga kwa hospitali zilizo jengwa kwa kodi ya watanzania- wasomali pia wanatoa na kukusanya kodi hakuna afya bora, elem wala siasa safi!

Waislamu wanabanwa na
mfumo kristo
- Somalia kuna mfumogani unaowabana wasiendelee



Original Source:
Jamii Forums Jukwaa La Siasa